Makamu Rais Joyce Banda ameapishwa kama rais wa Malawi Jumamosi kufuatia uthibitisho wa serikali kuwa Rais Bingu wa Mutharika alifariki dunia ghafla Alhamisi.
Banda, anakuwa mwanamke wa kwanza kuwa rais Malawi ameingia madarakani kama inavyosema katiba ya nchi hiyo. Alikula kiapo katika mji mkuu, Lilongwe.
Serikali ya Malawi ilitangaza rasmi kifo cha rais wa nchi hiyo Bingu wa Mutharika baada ya siku tatu tangu kitokee. Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Banda alisema ameshtushwa na kusikitishwa sana na kifo cha Mutharika.
Maafisa wa serikali wanasema Mutharika alipata na mshtuko wa moyo Aprili 5 katika makazi ya rais na kukimbizwa katika hospitali kuu ya Kamuzu mjini Lilongwe.
Banda alisema kuwa matayarisho ya maziko yatatangazwa baadaye baada ya kushauriana na familia ya Bwana Mutharika.